Wawekezaji wa migodini sasa kuchunguzwa
Written By Unknown on Saturday, 15 September 2012 | 09:38
WIZARA ya Nishati na Madini imeunda jopo la wasomi na wataalamu saba kwa ajili ya utafiti wa kuwachunguza wawekezaji waliopo katika migodi yote nchini, kama wanatimiza masharti ya leseni wanazopewa.
Jopo hilo lilitangazwa jana mbele ya waandishi wa habari Dar es Salaama na Kaimu Kamishna wa Madini, Ally Samaje na kuliagiza jopo hilo kuanza kazi hiyo leo katika migodi iliyopo mkoani Arusha.
Walioteuliwa ni pamoja na Dk. Rumisha Kimambo, Dk. Agostino Hangi, Dk. Wilson Mutagwasa, Profesa Samwel Wangwe, Punzi Juma, Neema Mwasulanga na Fortunata Kenyunko.
“Kutokana na kuwapo na migogoro mingi katika migodi yetu, tumeona ni vema tukafanya utafiti kujua kwa undani kwa nini wawekezaji na wananchi wamekuwa katika mvutano na kusababisha mauaji.
“Tunataka kujua wawekezaji hawa wanatoaje fursa kwa wananchi wanaozunguka migodi hiyo, wanachangia vipi maendeleo ya vijiji kama ujenzi wa shule, visima, barabara, vituo vya afya na huduma zote za kijamii.
“Pia tunataka kujua kwa nini kunatokea migogoro ya mara kwa mara na hata kusababisha vifo vya wananchi, baada ya kupata majibu ya jopo hilo tutajua namna ya kuondoa hali hiyo. Vile vile wawekezaji watakaokuwa wanatekeleza masharti ya leseni zao watapewa tuzo,” alisema.
Samuje alisema jopo hilo litafanya utafiti katika migodi mikubwa minane na midogo kumi na kusema kuwa matokeo ya utafiti huo yatatangazwa Desemba mwaka huu. Alisema wakati wa utafiti katika mgodi husika, jopo hilo litakuwa linawahusisha wananchi wa eneo hilo, ili kupata ukweli kama wawekezaji wanatoa fursa kwao.
Hata hivyo alitoa angalizo kwa jopo hilo kutojihusisha na kupokea rushwa kutoka kwa wawekezaji, ili kuficha ukweli na kuongeza kwamba kama watadiriki kuhongwa wataendelea kuwaangamiza Watanzania, huku wageni wakiendelea kufaidika na rasilimali za taifa.
Labels:
mchanganyiko,
mpya,
siasa
0 comments:
Speak up your mind
Tell us what you're thinking... !